HAYA! Alexis Sanchez huyo hapo, mchukueni! Arsenal imesema hivi, staa huyo wa Chile atakuwa huru tu kwenda kwenye timu yoyote anayotaka kama tu itawekwa Pauni 35 milioni mezani.
Kwa lugha nyepesi tu. Arsenal inampiga bei staa wake huyo kwa Pauni 35 milioni. Ndiyo, Pauni Thelathini na Tano milioni tu.
Sanchez aligomewa kwenda Manchester City kwenye dirisha lililopita na kocha Arsene Wenger alidai kwamba hamuuzi kwenye dirisha la Januari, lakini kwa sasa anaonekana kuanza kulegeza masharti.
Kwa sababu mkataba wa mchezaji huyo utafika tamati mwisho wa msimu na kwamba ataondoka bure, Arsenal kwa sasa wamemua ni heri wakaambulia chochote kuliko kumshuhudia mchezaji huyo mahiri kabisa kuondoka bila ya kupata chochote.
Kutangazwa kwa dau hilo kuna maana kwamba sasa Manchester City, Paris Saint-Germain, Bayern Munich na timu nyingine zinazohitaji huduma yake ni wakati wao tu kuanza kupeleka ofa zao kwa ajili ya kupata huduma yake.
Mchezaji mwenyewe anataka kuachana na Arsenal kwa haraka iwezekanavyo na anachoombea ni Man City wapeleke hizo Pauni 35 milioni.
Arsenal imeripotiwa kutangaza bei hiyo kwa sababu tu inataka mteja wa haraka Januari huku wakipanga kumharibia staa huyo baada ya kudaiwa kwamba, amepanga kujiunga na Man City mwishoni wa msimu ili akapewe mkataba wenye thamani ya Pauni 400,000 kwa wiki.
Uamuzi huo ina maana timu yoyote itakayoleta mkwanja ambao, Arsenal inataka kwenye dirisha la Januari, basi Sanchez anapigwa bei.
Maoni
Chapisha Maoni