Meneja wa Manchester United Jose Mourinho ameendeleza vita ya meneno dhidi ya bosi wa Chelse Antonio Conte, akikumbushia adhabu ya Muitaliano huyo 2012 kwa kupanga matokeo.
Mameneja hao wawili wameingia kwenye mgogoro siku mbili zilizopita Conte akisema kuwa Mourinho ana tabia ya "utovu wa nidhamu pembezoni mwa chaki".
Msemo huo wa Conte aliutoa akimjibu Mourinho aliyebwata kuwa baadhi ya mameneja wa Premier League wana tabia "kama kijana chizi" wakati wa mechi - kauli ambayo ilimlenga bosi wa Chelsea.
Muitaliano huyo alidai kuwa Mourinho alikuwa akisumbuliwa na ugonjwa mbaya wa kupoteza kumbukumbu, akitaja kwa msamiati wa Kiitaliano akimlenga bosi wa Man United.
"Nadhani anahitaji kujichunguza alivyokuwa huko hapo awali - labda alikuwa akijizungumzia alivyokuwa siku za nyuma," alisema Conte. "Labda, wakati mwingine, nadhani anasahau alichowahi kusema zamani, jambo ambalo ni tabia yake.
"Wakati mwingine nadhani analo tatizo, silijui jina, lakini demenza senile... pale unaposahau kile ulichokifanya wakati uliopita.
Baada ya Manchester United kushinda 2-0 dhidi ya Derby County kwenye mechi za Kombe la FA Ijumaa, Mourinho alifufua upya uhasama wao.
"Jambo pekee ninalotaka kusema kumaliza habari ni ndiyo, niliwahi kufanya makosa siku za nyuma kwenye mstari wa chaki," alisema Mourinho.
"Naam, nitapunguza, lakini nadhani bado nitaokesea kidogo. Jambo ambalo halijawahi kunitokea na kamwe halitatoke ni kufungiwa kwa kupanga matokeo.
"Hilo halijatokea kwangu na kamwe haitatokea."
Kauli za Mourinho zinarejea adhabu ya kufungiwa mechi nne aliyopewa Conte msimu wa 2012-13 akiwa meneja wa Juventus kwa kushindwa kutoa maelezo ya kupanga matokeo akiwa akiiongoza Siena.
Maoni
Chapisha Maoni